WEZI WA MAJI : NAIBU WAZIRI WA MAJI MHE. AMOS MAKALLA AWANASA WEZI WA MAJI DAR NA KUTANGAZA KUFILISI MALI ZAO - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


15 Jul 2014

WEZI WA MAJI : NAIBU WAZIRI WA MAJI MHE. AMOS MAKALLA AWANASA WEZI WA MAJI DAR NA KUTANGAZA KUFILISI MALI ZAO



Meneja Mkuu wa Kampuni ya ufyatuaji matofali ya Ujenzi Solutions, ya Kimara kwa Msuguri, Dar es Salaam, Rahim Hamis na mfanyabiashara wa kampuni isiyo na jina, Credo Rajab (kulia) wakiwa chini ya uliznzi wa Polisi huku wakiwa wamevishwa pingu baada Naibu Waziri wa Maji, Amos Makalla kuamuru kuwakamata alipokagua viwanda vyao vya ufyatuaji na kugundulika kuwa wanatumia maji isivyo halali kwa kujiunganishia kwenye bomba kuu la Mamlaka ya Maji Safi na Taka Dar  ws Salaam (DAWASA).  Makalla ambaye alifanya ziara ya kukagua maendeleo ya upanuzi wa Matambo wa Maji wa Ruvu Juu, Mlandizi, mkoani Pwani , pia alifanya msako wa kushitukiza kwa kampuni hizo.
Naibu Waziri wa Maji, Amos Makalla (kulia) akijaribu kuendesha katapila la Kampuni ya Ujenzi ya VA Tech Wabag Ltd, alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya upanuzi wa Mitambo ya Maji ya Ruvu Juu, Mlandizi, mkoani Pwani .Katikati ni Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini, Hamoud Jumaa na Meneja Mradi wa kampuni hiyo, Pintu Dutta.
Askari wa FFU wakilinda doria katika kiwanda cha ufatuaji tofali cha Ujenzi Solutions, Kimara Dar es Salaam
Moja ya mabomba linalodaiwa kuunganishwa kiholela kwenye bomba kuu la Ruvu Juu linaloleta maji  mjini na kampuni ya Ujenzi Solutions eneo la Kimara
Makalla akizungumza mbele ya Lori la Maji lililokamatwa likijazwa maji yanayodaiwa kuwa ya Dawass, katika kiwanda cha matofali cha Ujenzi Solutions







Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini, Hamoud Jumaa akijaribu kuendesha katapila la Kampuni ya Wagani ambayo imepewa tenda ya upanuzi wa Mtambo wa Maji wa Ruvu Juu.
Makalla (wa pili kushoto) Mbunge wa Kihaha Vijijini, Hamoud Jumaa ( wa pili kulia) na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Halima Kihemba kulia, wakikagua ujenzi wa upanuzi wa mtambo huo. PICHA ZOTE NA KAMANDA WA MATUKIO BLOG


 Na Richard Mwaikenda

NAIBU Waziri wa  Maji, Amos Makalla amezifungia kampuni tatu za ufyatuaji tofali kuendesha shughuli baada ya kubainika  kujiunganishia isivyo halali maji kutoka kwenye bomba kuu la Mamlaka ya Maji Safi na Taka (DAWASA), wakati wa ukaguzi wa kushitukiza alioufanya leo katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Makalla aliamuru viongozi wa kampuni  hizo wakamatwe na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kwa hatua zaidi, ambapo pia aliagiza mali zote za kampuni hizo zifilisiwe ili zitumike kulipa fidia kwa hasara kubwa iliyoingizia Serikali.

Akiwa katika ukaguzi huo, Makala aligundua madudu mengi yanayofanywa na kampuni hizo, ambazo zimejiunganishia maji kwa ajili ya kufyatulia matofali na kuuza kwa kutumia malori.

Kampuni alizozikagua leo na kukutwa na dhahama hiyo ni; Moto iliyopo mita chache kutoka Makao Makuu ya Wizara ya Maji, Ubungo Dar es Salaam, Ujenzi Solutions iliyopo Kimara kwa Msuguri pamoja na kampuni isiyo na jina iliyopo pia Kimara kwa Msuguri.

Kabla ya kufika katika kampuni hizo, ulinzi wa Polisi wenye silaha ulikuwa umeimarishwa, ambapo Makalla alitoa agizo kwamba wasiondoke katika maeneo hayo ili wahusika na wafanyakazi wao wasiendelee na kazi yoyote.

Katika kampuni ya Moto, ilikutwa pampu ikiendelea na kazi ya kuvuta maji ambapo Msimamizi wa kampuni hiyo, Frederick Tarimo alikana kuiba maji kwenye bomba la Dawasa na kudai kwamba maji hayo wanayatoa kutoka kwenye mto.

Tarimo alisema kuwa hutumia lita 3000 za maji kwa siku, ambapo hufyatua matofali kati ya 1500 na 2000 kwa siku. Pia huuza kwa siku kiasi cha matofali kama hayo. Kila tofari huuzwa kati ya sh. 800 na 1000. Alisema kuwa endapo hatofanya kazi kwa muda wa mwezi mmoja ataingia hasara ya sh. mil. 90, hivyo kila siku kupata hasara ya sh. mil. 3.

Naye Meneja wa kampuni ya Ujenzi Solutions, Rahim Hamis, alikana katakata kwamba maji wanayoyatumia wameunganisha kutoka kwenye bomba la Dawasa, bali wanatumia maji kutoka kwenye bwawa dogo lililopo jirani na kampuni yao. Pia katika eneo hilo lilikamatwa lori  aina ya Isuzu namba 957 AJK likijazwa maji.

Viongozi waliokamatwa ni Frederck Tarimo ambaye alijitaja kuwa msimamizi wa kampuni ya Moto, Meneja Mkuu wa kampuni ya Ujenzi Solutions, Rahim Hamis na Credo Rajab mmiliki wa kampuni aliyodai haina jina.

Makalla, alisema ili kupambana na wezi wa maji, haina budi sasa kupeleka mswada bungeni ili watungiwe sheria ya uhujumu uchumi pamoja na kutoa adhabu kali ikiwemo ya kutaifisha mali zao, tofauti na adhabu wanayopewa sasa ya kulipishwa faini ya sh, mil 2.

Katika ziara hiyo pia alifanya ukaguzi wa matanki ya kuhifadhia maji ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo alijionea jinsi maji yalivyopungua kwenye matanki hayo ambayo pia yapo kwenye maandalizi ya kufanyiwa ukarabati mkubwa ili yafae kwa ajili ya hifadhi ya maji kutoka bomba la Ruvu Chini ambalo upanuzi wake umekamilika.

Pia alitembelea kuona maendeleo ya upanuzi wa Mtambo wa Maji wa Ruvu Juu, Chalinze, Mkoa wa Pwani. kesho anaendelea tena na ziara kama hiyo katika Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad