ELIMU YETU :ELIMU YA URAIA NA UPIGAJI KURA HAIPASWI KUWA NA UTASHI WA KISIASA WALA UPENDELEO - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


16 Oct 2014

ELIMU YETU :ELIMU YA URAIA NA UPIGAJI KURA HAIPASWI KUWA NA UTASHI WA KISIASA WALA UPENDELEO

DSC_0087
Afisa Miradi ya Mawasiliano, Habari na Tehama wa shirika la kimataifa la sayansi, elimu na utamaduni (UNESCO) Bwana Al Amin Yusuph akielezea madhumuni ya warsha ya wadau wa mradi wa uchaguzi 2015 unaolenga kuboresha demokrasia amani nchini katika kipindi hiki kuelekea uchaguzi mkuu ujao, unaofadhiliwa na Shirika La Kimataifa la Maendeleo (UNDP) ulioenda sambamba na mkutano wa tano wa Mtandao wa vyombo vya habari vya Kijamii nchini (COMNETA).
*********************************************
Na Mwandishi wetu
Uchaguzi huru na wa haki utafanikiwa iwapo wananchi watapewa elimu sahihi ya uraia na upigaji kura itakayohamasisha wapiga kura kufanya maamuzi sahihi wakati wa uchaguzi.
Hayo yamesemwa na Kamishna wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Jaji John Mkwawa kwenye washa ya siku nne ya wadau wa utekelezaji wa mradi wa uchaguzi unaolenga kuboresha demokrasia na amani nchini kuelekea uchaguzi mkuu ujao .
Kamishina alisema elimu ya uraia ni muhimu kwa wananchi ili kuwahamasisha ushiriki wao katika demokrasia na kwamba haipaswi kuwa na utashi wa kisiasa au upendeleo kwa chama chochote cha siasa.
Akitoa mada katika warsha hiyo inayofadhiliwa na shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia maendeleo (UNDP) Jaji Mkwawa alisema katika kutoa elimu hiyo wanahabari hawana budi pia kuzingatia miongozo iliyowekwa ya kutofungamana upande wowote kisiasa na kutoa habari kwa usahihi kuhakikisha kwamba makundi yote yanapewa fursa na haki sawa.
DSC_0124
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo (UNDP) Godfrey Mulisa akisoma risala ya ufunguzi wa warsha hiyo kwa niaba ya Philippe Poinsot inayoendelea kwenye ukumbi wa mikutano ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma.
***************************************
“Pamoja na changamoto zinazozikabili redio jamii, zina mchango mkubwa katika mchakato wa uchaguzi kwa sababu idadi kubwa ya Watanzania hawajui kusoma na kuandika hivyo kutegemea redio. Kwa misingi hiyo ni vyema kwa waandishi wa habari wa redio jamii kusaini mwongozo wa maadili ambayo yataonyesha utekelezaji wao kwa kutopendelea chama chochote cha siasa au mgombea yoyote yule ”.
Amependekeza pia umuhimu wa kuielewa jamii inayolengwa wakati wa kutayarisha vipindi vya elimu ya uraia na utekelezaji ili taarifa zinazotolewa kwao zikidhi matakwa ya sehemu hiyo.
Kamishna wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji John Mkwawa ametoa mfano wa kuilewa jamii kuwa ni pamoja na kufahamu sababu zinazowafanya wananchi wasijitokeze kwa wingi katika upigaji kura iwapo kunasababishwa na ukosefu wa taarifa muhimu na sahihi, kukosa motisha ya kupiga kura, utashi na kutokuwepo kwa ushindani katika kugombea.
“Katika uchaguzi mkuu mwaka 2010 watu wachache sana walijitokeza kupiga kura pamoja na jitihada zote za kuhamasisha na kuelimisha upigaji kura, na baadhi ya sababu ni kwamba kupiga kura hakutampa faida yoyote mpiga kura, au kupiga kura hakutaleta mabadiliko yoyote na kutouamini mfumo mzima wa uchaguzi”.
DSC_0005
Mwenyekiti wa mtandao wa vyombo vya habari vya kijamii Tanzania (COMNETA) ambaye pia ni Mkurugenzi wa Redio ya Jamii FADECO wilayani Karagwe, Bw.Joseph Sekiku akieleza kwa ufupi maendeleo ya COMNETA wakati wa sherehe za ufunguzi za mkutano wa tano wa Mtandao wa vyombo vya habari vya Kijamii nchini (COMNETA) unaofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad