Maisha na Utalii : KINUKAMORI Waomba dola 30,000 Kutengeneza Ajira kwa Watu 300, Moshi-Kilimanjaro - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


12 Nov 2014

Maisha na Utalii : KINUKAMORI Waomba dola 30,000 Kutengeneza Ajira kwa Watu 300, Moshi-Kilimanjaro


DSC_0218
Mkurugenzi Mtendaji wa EWP na Mkurugenzi wa Kinukamori Enterprises, Bw. Alpha Phares Moshi (wa pili kushoto) akimkaribisha Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la maendeleo UNDP, Alvaro Rodriguez alipowasili kwenye Taasisi isiyo ya kiserikali inayo shughulika na uhifadhi wa mazingira eneo la Kinukamori, Marangu mkoani Kilimanjaro wakati wa ziara yake ya kukagua miradi mbalimbali inayofadhiliwa na UNDP huku akiwa amembatana na Mratibu wa Kitaifa miradi ya COMPACT mkoani Kilimanjaro, Victoria Nderumaki (wa tatu kulia) pamoja na Mtaalam wa Mahusiano na Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa (UN) Tanzania Hoyce Temu (wa pili kushoto).

Na mwandishi wetu, Moshi
Taasisi isiyo ya kiserikali inayo shughulika na uhifadhi wa mazingira eneo la Kinukamori, Marangu mkoani Kilimanjaro Executive Wilderness Program (EWP) inatafuta dola za marekani 30,000 kwa ajili ya kuendesha program tatu zenye kutengeneza ajira, ujasirimali, utunzaji wa mazingira na mvuto kwa watalii wanaokwenda kupanda mlima Kilimanjaro.
Kauli hiyo wameitoa kwa Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la maendeleo UNDP, Alvaro Rodriguez wakati alipofanya ziara mkoani Kilimanjaro kuangalia miradi inayofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).

Uongozi wa EWP and Kinukamori Enterprises katika taarifa yao kwa Mratibu huyo, iliyosomwa na Mshauri wao wa fedha Grace Shayo wamesema pamoja na nia yao ya kuhakikisha maporomoko ya Kinukamori yanaendelea, kwanza kama taasisi na pili kama mradi wa kuhifadhi mazingira ya Mlima Kilimanjaro ambao ni sehemu ya urithi wa dunia, wakishirikiana na KINAPA wamefikiria miradi kadhaa ambayo ikienda kwa pamoja itaendeleza eneo hilo.

Wamesema fedha hizo zitatumika kutoa elimu ya ujasirimali kwa vijana 300 wanaoishi katika jamii ya Marangu ambao hutoa huduma mbalimbali kwa wenyeji na pia wageni wakiwemo watalii. Kundi hilo linalotakiwa kupewa mafunzo ni pamoja na wapagazi 50, waendesha pikipiki 100, wachuuzi 100 na walima mboga 50.

DSC_0221
Mshauri wa fedha wa EWP na Kinukamori Enterprises, Grace Shayo akisalimiana na Mratibu miradi ya UNDP Kitaifa, Nehemia Mususuri aliyembata na Bw. Alvaro Rodriguez. Katikati ni Mkurugenzi Mtendaji wa EWP na Mkurugenzi wa Kinukamori Enterprises, Bw. Alpha Phares Moshi.

Pia fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kuanzisha na kutoa huduma ya chakula kwa wanaopanda mlima Kilimanjaro kwa lengo la kupunguza uchafu katika mlima huo na wakati huo huo kuongeza ajira kwa vijana. Aidha fedha hizo zitatumika kuanzisha kituo cha mazoezi kwa ajili ya wageni wanaotaka kupanda mlima Kilimanjaro kujizoesha na hali ya eneo hilo kabla ya kupanda mlima. Grace alisema shughuli zote hizo zimelenga vijana kuwa na maeneo ya kudumu yenye ajira endelevu.

Pamoja na kutoa ombi la kusaidiwa kupata fedha hizo, wameshukuru pia kwa misaada iliyotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP) kwa kupitia COMPACT.Wamesema kama si misaada hiyo eneo hilo ambalo lina historia ya kuharibiwa kwa mazingira yake lisingekuwa linavutia na kutoa ajira kama ilivyo sasa.

Eneo hilo limeboreka mazingira baada ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo ya EWP kazi iliyofanywa na Bw. Alpha Phares Moshi ambaye kwa sasa ndiye Mkurugenzi Mtendaji wa EWP na Mkurugenzi wa Kinukamori Enterprises ambapo kwa kushirikiana na KINAPA na COMPACT vijana walipewa elimu iliyowezesha kutengenezwa kwa mradi wa kuhifadhi mazingira ya mto Una wenye maporomoko ya Kinukamori.
DSC_0231
Bw. Alvaro Rodriguez akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili kwenye mradi huo.

Vijana hao ambao ndio wanaoishi katika mteremko wa mlima Kilimanjaro walianza shughuli hizo mwaka 1997 na kuanza kufikiria kuyatengeneza maporomoko ya Kinukamori kama chanzo cha kivutio katika juhudi za kuhifadhi mto Una.

Walisema kwa kuzingatia madhumuni ya kuanzishwa kwa mradi huo vijana na wanawake walianza kurejesha hali ya mazingira kwa kuyaweka bora na kudhibiti uharibifu wa ikolojia.
Kutokana na juhudi hizo miti zaidi ya 5000 mingi ikiwa ya asili ilipandwa kandoni mwa mto na sasa miti hiyo inatumika kutoa mafunzo na kurejesha hali ya upatikanaji wa maji ya kutosha kwa ajili ya wananchi wa Marangu.

Aidha wanyama na ndege waliokuwa wametoweka kutokana na uharibifu wa mazingira uliokuwepo kwanza wameshaanza kurejea eneo hilo.
Pamoja na mafanikio hayo EWP wanakabiliwa na changamoto kubwa hasa ukubwa wa eneo la shughuli zao ambalo ni ndogo na sasa wanataka kusaidiwa kufika hadi maeneo ya chemchem ya Soko iliyopo Kahe.
DSC_0262
Mshauri wa fedha wa EWP na Kinukamori Enterprises, Grace Shayo akisoma taarifa ya taasisi yao kwa Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la maendeleo UNDP, Alvaro Rodriguez.

Aidha wamesema wanakabiliwa na tatizo la fedha na hasa kushawishi vijana kujikita zaidi katika masuala ya uhifadhi wa mazingira na utalii wa kitamaduni. Naye Mwakilishi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa pamoja na kuwapongeza EWP kwa kufanikisha kurejesha mazingira katika hali ya kawaida katika eneo hilo amesema kwamba wataendelea kushirikiana nao kuhakikisha kwamba shughuli za hapo zinahifadhi mazingira na kutoa ajira kwa vijana.

Alisema duniani nzima kwa sasa inakabiliwa na tatizo la ajira kwa vijana ambao kutokana na kukosekana kwa ajira wanatopea katika ulevi na hivyo kuhatarisha nguvu kazi hiyo muhimu.
Alisema hata Tanzania pamoja na kuanza kufikiria kuwa na uchumi wa gesi, hatua hiyo itachukua muda lakini kuna haja ya vijana wanaomaliza shule wakawajibika katika miradi mbalimbali ya uhifadhi na maendeleo ya kiuchumi.
DSC_0271
Mshauri wa fedha wa EWP na Kinukamori Enterprises, Grace Shayo akikabidhi taarifa ya taasisi hiyo kwa Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la maendeleo UNDP, Alvaro Rodriguez aliyetembelea mradi wao na kujionea maendeleo yao.

Mwakilishi huyo pamoja na kutotoa ahadi katika ombi la taasisi hiyo amesema kwamba wataangalia nini cha kufanya kwani alifika eneo hilo kujifunza na kuona maendeleo kwani ana miezi miwili tu toka ameingia nchini kuwakilisha mashirika ya Umoja wa Mataifa.Alisema amefurahishwa na maendeleo yaliyopo na hasa kwa kuzingatia kwamba kulikuwa na tatizo la raslimali kufanya shughuli hiyo.

Alisema anatambua changamoto zilizopo cha ongezeko la watu, tatizo la ajira kwa vijana na mabadiliko ya tabia nchi na kwamba wataendelea kushirikiana na taasisi hiyo kuona kwamba changamoto hizo zinakabiliwa na kufutwa.
DSC_0228
Bango linaloonyesha tarehe ya kuzinduliwa kwa mradio huo wa COMPACT unaofadhiliwa na UNDP.
DSC_0455
Baadhi ya sheria zilizowekwa kwenye maporomoko ya maji ya Kinukamori yaliyopo Marangu mkoani Kilimanjaro.
DSC_0238
Mtaalam wa Mahusiano na Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa (UN) Tanzania Hoyce Temu akiwa amefuatana na Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la maendeleo UNDP, Alvaro Rodriguez kutembelea mazingira ya taasisi hiyo pamoja na vivutio vya kitalii vilivyomo kwenye Maporomoko ya maji ya Kinukamori yaliyopo Marangu mkoani Kilimanjaro.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad