Uchumi Wetu :Miundombinu ya Bandari ya Kigoma Kuboreshwa na Kupanuliwa - Wazalendo 25 Blog

Habari Mpya

Glory to Story.


Post Top Ad


12 Dec 2014

Uchumi Wetu :Miundombinu ya Bandari ya Kigoma Kuboreshwa na Kupanuliwa


 Mkuu wa Bandari ya Kigoma, Bw. Athuman Malibamba (Kulia) akimkaribisha Kiongozi wa Timu ya Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri (Kushoto) mara alipofika kujionea maendeleo ya bandari hiyo.
 Sehemu ya chelezo zinazotumika kwa ajili ya matengenezo ya meli na boti katika Bandari ya Kigoma.
 Mkuu wa Bandari ya Kigoma, Bw. Athuman Malibamba (Katikati mbele) akifafanua jambo kwa Timu ya Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango mara walipofika kujionea shughuli za maendeleo kiwanjani hapo.
Kiongozi wa Timu ya Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri (Aliyenyanyua mkono) akionesha kufurahia jambo wakati walipofanya ziara katika Bandari ya Kigoma.
 Mkuu wa Bandari ya Kigoma, Bw. Athuman Malibamba (Wapili kulia) akifafanua jambo kwa Timu ya Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango mara walipofika kujionea shughuli za maendeleo kiwanjani hapo.
Boti na meli zikipandisha shehena kwenye Bandari ya Kigoma.
PICHA ZOTE NA SAIDI MKABAKULI
Serikali imeazimia kuendelea kuboresha miundombinu ya bandari hususan miradi iliyoibuliwa katika Programu ya Matokeo Makubwa Sasa ikiwemo kuanza kufanya upanuzi wa Bandari ya Kigoma  na kuendelea kuboresha miundombinu na ununuzi wa vifaa mbalimbali vya kuhudumia shehena katika Bandari ya Kigoma ili kuweza kukidhi mahitaji yanaongeza siku baada ya siku katika bandari hiyo.
Ahadi hiyo imetolewa na Kiongozi wa Timu ya Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri wakati walipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya miundombinu katika Bandari ya Kigoma.
Bibi Mwanri alisema kuwa serikali kupitia Mamlaka ya Bandari nchini nchini ipo kwenye mkakati wa kuiendeleza bandari hiyo ili iwe ya kiwango kizuri kwa kuhudumia watumiaji wa wa bandari hiyo.
“Kama munavyokumbuka Serikali katika mwaka huu wa fedha ilipanga kuiendeleza na kuboresha miundombinu ya usafiri wa majini na anga ili kuongeza ufanisi wa sekta hizi, ambapo Bandari ya Kigoma ni mojawapo ya bandari zilizopewa kipaumbele kwa ajili ya uendelezaji,” alisema Bibi Mwanri.
Kwa mujibu wa Bibi Mwanri, upanuzi wa bandari hiyo upo kwenye hatua za upembuzi yakinifu kwa ajili ya kuboresha bandari ya Kigoma na kutwaa maeneo zaidi kwa ajili ya upanuzi wa bandari hiyo.
Akitoa taarifa ya maendeleo ya Bandari hiyo, Mkuu wa Bandari hiyo Bw. Athuman Malibamba alisema kuwa mpaka kufikia Juni 2014 hatua ya utekelezaji iliyofikiwa ni kukamilika kwa kazi ya uthamini wa mali eneo la Kibirizi lenye hekta 10 kwa ajili ya upanuzi wa bandari hiyo. “Pia, Mamlaka imempata Mtaalam Mshauri (M/S Royal Haskoning H.D.V Nederland, B.V) atakaefanya kazi ya Upembuzi Yakinifu. Aidha, kazi ya uthamini wa mali imekamilika kwa eneo la Katosho lenye hekta 69 kwa ajili ya kujenga bandari kavu,” alisema.
Kuongezeka kwa shughuli za kiuchumi katika nchi za jirani kunatoa fursa ya kuimarisha miundombinu ya bandari ya Kigoma ili kuwa na uwezo wa kuhudumia shehena inayoongezeka na kukuza uchumi katika mkoa na Taifa kwa ujumla. Aidha kuanzishwa kwa Eneo Maalum la Kiuchumi, katika mkoa wa Kigoma ni kichocheo muhimu kwa Mamlaka ya Bandari (TPA) kuimarisha huduma katika bandari ya Kigoma na hivyo kuweza kuzitumia fursa zitakazojitokeza mara baada ya shughuli mbalimbali za kiuchumi kuanzishwa.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad